Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Barabara ya Msumi nayo inangoja maagizo?

Ef1bebc74c323b609671dc1570e6578f.png Barabara ya Msumi nayo inangoja maagizo?

Fri, 22 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

MOJA ya majukumu ya Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini(Tarura) ni ujenzi na matengenezo ya mtandao wa barabara za vijijini na mijini ambayo hapo awali yalikuwa yakitekelezwa na Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Baada ya Tarura kupewa majukumu hayo rasmi mwaka 2017,ambayo mengine ni usimamizi, ujenzi, na matengenezo ya mtandao wa barabara za vijijini na mijini ikijumuisha kuimarisha usalama wa barabara, kulinda hifadhi za barabara zisivamiwe na kudhibiti athari za mazingira na za kijamii ilitegemewa kuwepo na maendeleo ya kasi kwenye barabara hizo.

Wananchi kwenye maeneo tofauti yanayohudumiwa na wakala huyo wanalia vilio ambavyo hawajui lini vitakoma na hiyo inatokana na ubovu wa miundombinu ya baadhi ya barabara za mitaa na vijijini na wakati mwingine zinazounganisha mji ambazo ziko chini ya Tarura.

Kwa wakazi wa Manispaa ya Ubungo, kero kubwa ni ubovu wa barabara nyingi za mitaa ambazo pamoja na Tarura kuzifahamu, hakuna shuluhisho la matatizo lililofanyika na hivyo kuwafanya watumiaji wa barabara hizo kuendelea kuwa watumwa ama wa kutembea umbali mrefu bila usafiri wa umma au kupanda usafiri mbadala ambao ni ghali kulingana na hali halisi ya maisha.

Mfano mzuri ni barabara ya Mbezi Louis kwenda Msumi, au Goba kwenda Msumi katika Manispaa ya Ubungo. Barabara hiyo licha ya kuwa ni kubwa na inayotambuliwa na Tarura, imekuwa kero kwa zaidi ya miaka 10 sasa huku ikisababisha huduma za usafiri wa umma kusuasua kwa sababu wamiliki wa magari hayo wanapata hasara kutokana na uchakavu wa barabara unaoharibu magari.

Licha ya Tarura kutambua ubovu wa barabara hiyo ya udongo inayowahudumia wananchi wengi waishio eneo la Msumi na maeneo jirani, ni kwamba haipitiki kipindi cha mvua na hata wakati wa kiangazi nako ni tatizo kutokana na mashimo na ubovu wake hivyo kufanya watumiaji kuteseka na usafiri kwa sababu wamiliki wengi wameacha kutoa huduma hiyo kwa kuhofia magari yao kuharibika.

Wananchi wanajiuliza, ni kweli hakuna viongozi wanaohusika na hizo barabara katika Wilaya hiyo ya Ubungo na Tarura hawaioni? Au wanasubiri hadi viongozi wa juu watoe maelekezo kama ilivyokuwa kwa Shule ya Msingi Kingóngo katika Manispaa hiyo hiyo?

Ifike mahali kila mtumishi awajibike kwa nafasi yake, ninaamini kuwa ubovu huo wa barabara ya Msumi na barabara nyingine ikiwemo ya Suca kwenda Golani katika Manispaa hiyo hiyo zinaweza kukarabatiwa iwapo Tarura wataamua kufanya hivyo badala ya kusubiri maagizo ya viongozi wa juu.

Kero ni nyingi zinazokwamisha maendeleo ya maeneo yetu ambazo ama kwa njia moja hazikupaswa ziwe kisababishi lakini kwa kuwa huenda kuna uzembe au baadhi ya watumishi kutotimiza wajibu wao inavyotakiwa, inasababisha kesho kwa jamii mzima.

Natumaini kwa viongozi wa Tarura watasikia, wachukue hatua kwa sababu kero hii ni kubwa kwenye maeneo mengi na hakuna hatua za wazi zinazoonekana kuchukuliwa kutatua tatizo.

Columnist: habarileo.co.tz