Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Akufaaye kwa dhiki ndiye rafiki

3411b142663ef40852f6f6b9c6e58c9e Akufaaye kwa dhiki ndiye rafiki

Fri, 16 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MWALIMU Julius Nyerere alifanya ziara yake ya kwanza ya kiserikali katika Jamhuri ya Watu wa China kutoka tarehe 16 hadi 23 Februari, 1965.

Rais Nyerere alipokewa vyema, na kuheshimiwa na wenyeji wake, Mwenyekiti Mao Zedong, Mwenyekiti Liu Shaoqi na Waziri Mkuu Zhou Enlai, kwa kuombwa kuhutubia katika mkutano mkubwa wa umati katika Uwanja wa Watu huko Beijing.

Mwalimu alisema: “Na sasa tuna rafiki, na rafiki mpya mkubwa, na rafiki ambaye tulifungamana pamoja naye kipindi cha ukoloni.

Hofu ya wengine, haitaathiri urafiki wa Tanzania na China, kama ilivyo kwa urafiki wetu na nchi nyingine hautaathiriwa na kile wapinzani wao wanasema juu yao.

“Imani yetu ni kwamba kila nchi lazima ichague aina yake ya jamii kulingana na hali yake inayokusudia. Imani hii ndiyo inayosababisha kupinga kwetu ukoloni na ukoloni mamboleo.

Tunataka kuwa rafiki wa wote, na kamwe hatutawaruhusu marafiki zetu wachague maadui zetu.” Ni kwa kufuata mafundisho haya, Tanzania inafurahi sana leo kama ilivyokuwa mwaka 1965, katika urafiki wake na China.

Nchi hizi mbili, chini ya uongozi wao, zamani na za sasa, bado zinaongozwa katika urafiki wao mkubwa, na mafundisho haya.

Fundisho hili lilikuwa msingi wa mkataba wa urafiki kati ya China na Tanzania, uliotiwa saini tarehe 20 Februari, 1965 kati ya Liu Shaoqi, Mwenyekiti wa Jamhuri ya Watu wa China, na Julius K. Nyerere, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mkataba huo una nakala tano, ambazo zinalenga kudumisha na kukuza uhusiano wa amani na urafiki kati ya nchi hizo mbili.

Mkataba huo unasema kwamba Tanzania na China zitadumisha kanuni tano za kuheshimiana katika uhuru wa kila mmoja na uadilifu wa eneo, kutokuchokozana, kutokuingiliana katika mambo ya ndani ya kila mmoja, usawa na faida ya pande zote, na kuishi kwa amani kama kanuni zinazoongoza uhusiano kati ya nchi mbili.

Pia mkataba unasema Tanzania na China zinakubali kuendeleza uhusiano wa kiuchumi na kiutamaduni katika ari ya usawa, kunufaishana na ushirikiano wa kirafiki, na kumaliza suala lolote linaloweza kutokea kati yao kupitia mashauriano ya amani.

Tunaposherehekea, Tanzania na China, mkataba huu wa kihistoria wa urafiki, tunapaswa pia kutoa pongezi kwa Jamhuri ya Watu wa China kwa msaada wote wa kiuchumi na kiufundi uliotolewa na China kwa Tanzania katika kipindi cha miaka 55 iliyopita. Imekuwa bado ni msaada mkubwa sana wa kirafiki.

Miongoni mwa msaada wote uliotolewa na China, ujenzi wa Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA) ulikuwa mchango mkubwa zaidi wa Wachina katika ukombozi wa kisiasa na kiuchumi wa Tanzania na Zambia.

Mradi huu unawakilisha upendo na heshima kubwa ya China kwa watu wa Tanzania, na kwa hakika Afrika kwa ujumla. Ulitolewa kwa Afrika kwa gharama kubwa na sehemu kubwa kwa njia ya kujitolea ya watu na serikali ya China.

Maombi yaliyotolewa na Rais Kaunda wa Zambia na Rais Nyerere wa Tanzania kwa nchi za Magharibi kwa ujenzi wa TAZARA yalikataliwa kabisa - wakati mwingine kwa dhihaka.

Balozi mmoja wa Marekani nchini Tanzania, wakati akijadili na Rais Nyerere juu ya ombi hili, alisema, “Bwana Rais, reli kwenda Zambia itapitia Zanzibar?” Hii ilimaanisha kuwa Tanzania ililazimika kukubali masharti ya kisiasa yanayoambatana na kutolewa kwa ombi hilo, mojawapo ikiwa ni kumaliza uwepo wa Zanzibar katika Ubalozi Mdogo wa Ujerumani Mashariki.

Hali hii haikubaliki kwa Tanzania. Kinyume chake, Serikali ya China na Chama cha Kikomunisti cha China chini ya uongozi wa Mwenyekiti Mao Zedong na Waziri Mkuu Zhou Enlai, mara moja walikubali ombi lililotolewa na Rais Nyerere na Rais Kaunda.

Mwenyekiti Mao alitaka kuhakikishiwa ikiwa reli ilikuwa inahitajika. Alipopata hakikisho hilo kutoka kwa Rais Nyerere, alijibu mara moja, “Itajengwa”. Hakuna masharti yaliyowekwa kwenye mradi huo mkubwa wa reli.

Mradi wa TAZARA na mingine mingi ikiwa ni pamoja na ile iliyo katika sekta ya kilimo na inayohusiana na amani na usalama wa nchi yetu, iliungwa mkono na China kwa msingi wa mkataba wa urafiki uliotiwa saini tarehe 20 Januari 1965.

Watu wa China, Tanzania, na mataifa mengine ya Kiafrika, tukumbuke historia na tushukuru, kwa njia ya pekee, baba waanzilishi wa mataifa yetu haya kwa uongozi wao na matamanio yao na hamu yao kwa ajili ya amani, umoja na mkakati wa maendeleo ya ninadamu.

China inabaki sasa kuwa rafiki wa kweli na muhimu kwa Tanzania na Afrika kwa ujumla. Mwandishi alikuwa Katibu Binafsi wa Rais Julius Nyerere na Ofisa Mkuu wa Ofisi ya Rais kutoka 1971 hadi 1985. Kwa sasa anahudumu kama Mkurugenzi.

Columnist: habarileo.co.tz