Msanii wa bongo fleva, Zuhura Othman 'Zuchu' amesema kuna wakati kwenye kazi zake, anajitolea mhanga na kubuni vitu ili kujifunza vitu tofauti na kukua zaidi kimuziki kama alivyofanya Simba Day.
Amezungumza hayo, wakati anafanya mahojiano na kipindi cha Refresh cha Wasafi Tv, amesema kitendo cha kushuka na kambi kwenye tamasha la Simba Day iliyofanyika Agosti 8, 2022 lengo lake lilikuwa ni kuacha historia kwa mashabiki.
"Sikuwa na uoga wowote, kwani tayari nilikuwa nimefanya mazoezi kama mara mbili, lengo langu ilikuwa ni kuzunguka na kamba uwanja mzima ili kuwafikia mashabiki wote, maana kukimbia unaweza usiyafikie maeneo mengine na ukawakwaza baadhi," amesema Zuchu.
Mbali na hilo, amewaondoa wasiwasi mashabiki wanaodhani wana bifu na msanii mwenzake Faustina Mfinanga 'Nandy', kwamba wanawasiliana tofauti na picha ya mashabiki wanaowashindanisha kimuziki.
"Sina tatizo lolote na Nandy na nilimpongeza baada ya kufunga ndoa, nadhani ni vile wanavyotushindanisha kwenye muziki na mimi niseme wazi sishindani na mtu kufanya kazi, bali napambana kufanya kazi zangu ziwe nzuri." amesema na kuongeza;
"Ninachotamani kukifanya nikuufanya muziki wangu uwe wa kimataifa, baada ya Watanzania kunipokea vizuri, hivyo wanahitaji kuona vitu vikubwa zaidi kutoka kwangu."