Dar es Salaam. Kesi ya kurekodi video ya ngono na kuisambaza katika mitandao ya kijamii inayomkabili mlimbwende wa Tanzania mwaka 2006, Wema Sepetu imekwama kuendelea ikielezwa kuwa mshtakiwa ni mgonjwa.
Hayo yameelezwa leo Jumanne Mei 14, 2019 na wakili wa utetezi, Ruben Semwanza mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Maira Kasonde.
Semwanza amesema akiwa mahakamani hapo alipewa taarifa kuwa Wema anaumwa.
"Taarifa nimepewa asubuhi hii nikiwa hapa mahakamani na mdhamini wake hayupo amenieleza yupo kikazi mkoani Arusha, hivyo naiomba Mahakama hii ipange tarehe nyingine," amedai Semwanza.
Wakili wa Serikali, Grory Mwenda amedai kuwa shauri hilo lipo kwa ajili ya kusikilizwa pia shahidi aliyetakiwa awepo kutoa ushahidi naye hayupo hivyo aliiomba tarehe nyingine kwa ajili ya kusikilizwa.
Baada ya maelezo hayo Hakimu Kasonde ameahirisha kesi hiyo hadi Juni 11, 2019 itakaposikilizwa.
Pia Soma
- Serikali ya Tanzania yatoa neno yanayoendelea Afrika Kusini
- Ukatili wa watoto waongoza kwa uvunjifu haki za binadamu
- Kesi ya Mbowe na wenzake yakwamisha kesi ya Halima Mdee