KUMEKUCHA Musoma,Walimbwende 16 wanatarajia kuchuana kuwania umalikia wa Miss Mara 2018 katika shindano linalotarajiwa kufanyika Julai 7 mjini humo.
Tayari Warembo hao wapo kambini kwenye Fukwe za Le Grand Beach mjini Musoma wakijifua vilivyo kusaka taji hilo la Mkoa wa Mara.
Msemaji wa Shindano hilo,Shomari Binda aliwataja Warembo hao kuwa ni Hawa Okoth,Merry Ibrahim,Ester William,Neema Charles Debora Shabani na Pricios Rahim.
Aliwataja walimbwende wengine kuwa ni Suzan Selemani,Rubb Vedastus,Sarah Emmanuel,Veronica Ogada,Neema Hosea,Evone Paul,Neema Noel na Nelly Alex.
Binda alisema Warembo wote wapo kambini ambapo kwa sasa wako katika maandalizi ya nguvu huku wakiwa kwenye ari nzuri ya ushindani.
Alisema mshindi wa shindano hilo atawakilisha Mara kwenye mashindano ya Miss Kanda ya Ziwa ambapo amesema wamejipanga kuhakikisha wanatoa mrembo Bora atakayeipa sifa mkoa huo.
“ Shindano la mwaka huu litakuwa zuri kutokana na kujipanga vizuri na imani iliyopo ni kila atakayekuja kushuhudia atafurahia na kumshuhudia mrembo atakayeuwakilisha mkoa wa Mara kwenye mashindano ya kanda ya Ziwa”alisema Binda.