MSANII wa muziki wa kizazi kipya, Vanessa Mdee amesema pamoja na kwamba Watanzania wanapitia wakati mgumu wakiwa na majonzi kwa kifo cha Rais wao mpendwa awamu ya tano, John Magufuli yapo matumaini mapya.
Kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram, Vanessa ambaye anaishi Marekani kwa sasa, amesema kuna matumaini ya kuwepo kwa mwanamke imara mwenye uwezo, Samia Suluhu Hassan ambaye ameapishwa kuwa Rais baada ya kifo cha Magufuli.
“Tunakukaribisha na kukupa salam Rais Mama Samia Suluhu, tumebarikiwa kushuhudia siku ambayo taifa letu linapata kiongozi wa kwanza mwanamke,” ameandika kwenye mtandao huo wa kijamii.
Nyota huyo ambaye ameacha kuimba muziki na kuhamia kwa mchumba wake Mmarekani mwenye asili ya Nigeria maarufu kwa jina la Rotimi, alisema anamuombea Rais Samia nguvu na ujasiri katika kutekeleza majukumu yake.