Dar es Salaam. Wakati msanii wa Bongofleva, Mbosso Khan akidai amezaa mtoto na msanii wa kundi la vichekesho la Cheka Tu, Martha Michael ‘Boss Martha’ Kaka wa marehemu Emmanuel Shilole, amesema atafunguka kuhusiana na suala hilo baada ya kumalizika kwa maziko.
Akizungumza na Mwananchi leo Septemba 13, 2019 kaka huyo ambaye amezaliwa tumbo moja na Boss Martha amesema ana hasira na yanayozungumzwa juu ya ndugu yao huyo.
Mara baada ya kufariki Martha msanii kutoka lebo ya Wasafi Mboso kupitia ukurasa wake wa Instagram aliandika kwa kirefu kuhusu kuumizwa na kifo cha mzazi mwenzake huyo.
Miongoni mwa mambo aliyoandika ni pamoja na kueleza kuwa walikubaliana wasizungumze kuhusu mtoto huyo kutokana na familia ya Martha kutopenda binti yao kuzaa na msanii.
Alipoulizwa kama jambo hilo lina ukweli au la alisema sasa sio muda wa kulizungumzia na kumuomba aachwe wamsitiri ndugu yao.
"Kama familia tumesikia mengi kuhusu ndugu yetu baada ya kufariki likiwemo hilo suala la kuwa na mtoto ambalo nina hasira nalo, lakini acha tumalize kuzika nitakuja kuliongelea," alisema Emmanuel.
Habari zinazohusiana na hii
- Mwili wa mchekeshaji Martha kuzikwa kesho Dar
- Marehemu Boss Martha alikuwa mzazi mwenzake msanii mbosso
Hata hivyo, aliiambia Mwananchi kuwa kama Mbosso anajiamini alizaa na mtoto wao kwa nini hakufuata taratibu za kitamaduni kama zinavyotaka.
"Pamoja na yaliyotokea kama ana uhakika aje mwenyewe katika familia atuambie kuhusu suala hilo badala ya kuzungunzia pembeni," alisema baba mdogo huyo aliyesema hiyo ndio mara yake ya kwanza kusikia kama ana mtoto.