Dar es Salaam. Wakati shindano la kumsaka mrembo wa dunia mwaka 2019 likitarajiwa kufanyika Jijini Londoni nchini Uingereza, Serikali ya Tanzania imesema itampatia kamusi za Kiswahili mwakilishi wa Tanzania atakapokwenda kwenye mashindano hayo.
Hayo yamesemwa jana Ijumaa Agosti 23,2019 na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe katika fainali za kumsaka Miss Tanzania zilizofanyika jijini Dar es Salaam.
Waziri Mwakyembe alisema mrembo wa Tanzania hana budi kujivunia lugha hiyo kokote anakokwenda ikiwemo katika shindano hilo litakalokutanisha nchi mbalimbali duniani na kuongea kuwa Serikali itampatia kamusi za Kiswahili kwenda nazo.
"Ili kuhakikisha mrembo watu anakitangaza vizuri Kiswahili, tutampatia kamusi nyingi za lugha hiyo ili akazigawe kwa warembo wenzake atakapokwenda nchi London kumsaka mrembo wa dunia ili nao waweze kujifunza lugha hiyo ambayo hivi karibuni imechaguliwa rasmi kuwa lugha ya nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Sadc)," alisema Dk Mwakyembe.
Hata hivyo, waziri huyo alisema anasikitishwa na kitendo cha warembo wanaoshiriki shindano la Miss Tanzania kuendelea kutumia lugha ya Kingereza kujieleza pale inapofika hatua ya kuulizwa maswali wakati wana uwezo wa kuzungumza Kiswahili vizuri.
Pia Soma
- Vigogo wa sheria UDSM waichambua Sadc
- Si kila mwenye ualbino ana saratani ya ngozi
- Vitambulisho vinavyokubaliwa katika uchaguzi wa serikali za mitaa hivi hapa
“Hii sio sahihi kwani aliyekuambia usipoongea Kingereza hautashinda nani, hebu warembo wetu wabadilike kupenda vya kwao," alisema Waziri Mwakyembe
Jaji Mkuu wa mashindano hayo, Shyrose Bhanji alisema hakuna mrembo anayelazimishwa kuzungumza Kingereza isipokuwa ni utashi wa muhusika kuamua atumie lugha ipi.