Dar es Salaam. Wakati sherehe ya kumbukumbu ya kuzaliwa mama wa msanii Diamond Platnumz na mpenzi wake Tanasha Donna, ikitarajiwa kufanyika leo jioni Jumapili Julai 7, 2019, maandalizi ya kupambana ukumbi wa Mlimani City itakapofanyika yameanza usiku wa kuamkia leo.
Mwananchi limefika katika ukumbi huo leo Jumapili Julai 7, 2019 mchana na kukuta timu ya watu 30 wakiwa wamejigawa kwa kazi mbalimbali za kuupamba ukumbi huo.
Kati yao wapo waliojishughulisha na kufunga jukwaa, vyombo vya muziki kupanga meza, viti na kutandika mazulia.
Mmoja wa wasimamizi wa Kampuni ya Hugo iliyopewa jukumu la kupamba, Shabani Kijio amesema wameanza kupamba usiku wa kuamkia leo.
Sherehe hiyo itakayofanyika leo jioni na kupewa jina la Gospy 707 imekuwa gumzo mitandaoni tangu Diamond alipoitangaza Julai mosi, 2019 na kutoboa siri kuwa mama yake na mpenzi wake huyo ambaye ni raia wa Kenya, wamezaliwa mwezi na tarehe moja.