Dar es Salaam. Msanii wa muziki wa Bongo Fleva nchini Tanzania, Naseeb Abdul maarufu Diamond amesema ana imani katika tamasha la Wasafi msanii Harmonize atashiriki.
Diamond ametoa kauli hiyo leo Jumatano Oktoba 30, 2019 siku chache baada ya kueleza kuwa anatakiwa kuilipa lebo ya Wasafi Sh500 milioni ili apate hakimiliki ya nyimbo na jina lake baada ya kujiweka kando na lebo hiyo.
Tamasha la Wasafi mkoani Dar es Salaam linatarajiwa kufanyika Novemba 9, 2019 katika viwanja vya Posta, Kijitonyama.
Diamond amesema Harmonize ni mtoto wa Wasafi hivyo ushiriki wake katika tamasha hilo hauna pingamizi lolote. Diamond amesema mbali na Harmonize kuwa na fursa ya kushiriki, pia ametuma mwaliko kwa uongozi wa msanii Ali Kiba akibainisha kuwa matamasha ya aina hiyo yanatakiwa kutumika kuondoa tofauti za wasanii.
"Wenzetu (wasanii) Nigeria ndio maana wanaendelea kwenye muziki kwani kunapokuwa na matamasha kama haya wanaweka tofauti zao pembeni, kumkuta jukwaa moja Wizkid na Davido ambao walikuwa na bifu kwao ni jambo la kawaida.”
“Kwa nini tung’ang’anie bifu hata sehemu ambayo ni ya kutengeneza pesa na kutuleta Watanzania pamoja,” amesema Diamond.
Kuhusu wasanii wanaoshiriki katika matamasha mengine amesema nao waruhusiwe kwa kuwa hiyo ndio sehemu yao ya kupata riziki, “ndio maana wasanii wa Wasafi hatujawabana kushiriki matamasha mengine.”