Dar es Salaam. Mwenyekiti mtendaji wa bodi ya mashindano ya Miss Utalii nchini Tanzania, Gidion Chipungahelo amesema usaili wa kuwasaka walimbwende wa shindano hilo utafanyika katika kanda sita.
Shindano la kumsaka Miss Utalii limerejea ikiwa ni miaka sita tangu lilipositishwa na Baraza la Sanaa la Taifa (Basata) kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kutakiwa kuendeshwa kama taasisi na si mtu mmoja kama alivyokuwa ikifanyika.
Akizungumza na Mwananchi jana Ijumaa Agosti 2, 2019 Chipungahelo amezitaja kanda hizo kuwa ni Kaskazini, Swahili Cost, Mashariki, Magharibi, Nyanda za juu kusini na Ziwani kati.
“Shindano hili litakuwa na nguzo kuu mbili ambazo ni kanda na Taifa, tutaanza usaili mwishoni mwa mwezi huu na tumeunganisha mikoa kulingana na kanda zilivyo,” amesema.
Julai 2, 2019 Chipungahelo alilieleza Mwananchi kuwa hivi sasa waandaaji wa shindano hilo wanatakiwa kuwa na elimu kuanzia shahada (degree).
Kwa uamuzi huo waratibu wa ngazi ya kanda wa shindano hilo wanatakiwa kuwa na elimu kuanzia shahada ili kupatiwa kibali cha uandaaji.