Ipo tabia ya baadhi ya watu kuwa na mawasiliano na watu wa jinsia nyingine, kwa madai kwamba ‘huyu ni rafiki yangu’.
Wakati mwingine inakuwa kweli kwamba hakuna chochote kibaya kinachoendelea kati yao, ni urafiki wa kawaida kabisa lakini je, ni sahihi kwa mtu ambaye yupo kwenye ndoa kuwa na ukaribu wa aina hii na mtu wa nje?
Unaishi na mkeo, kwa nini unaendeleza mawasiliano na wanawake wa nje? Hata kama hakuna chochote kati yenu, kwa nini unawapa muda wako?
Kwa nini unawaruhusu wavuruge amani iliyopo ndani ya ndoa yako? Kwa wanawake pia, unaishi ndani na mumeo. Kwa nini unakuwa na mazoea na wanaume wa nje kwa kisingizio cha ‘nilisoma nae’, au ‘ni mpenzi wa rafiki yangu’?
Simu yako kutwa iko bize, mara dereva wa bodaboda anayekubeba anakuuliza maswali yasiyohusiana na kilichowakutanisha, mara muuza bucha anakuuliza kama akuwekee mboga gani na mambo mengine mengi yenye kuudhi.
Kwa nini unakosa nidhamu na matumizi ya simu yako? Wasichokijua watu wengi ni kwamba kuwa na mazoea na watu wa jinsia nyingine wakati upo kwenye ndoa, ni jambo la hatari ambalo ukilichekea, linaweza kusababisha hata ndoa yako ikavunjika kimasihara.