Dar es Salaam. Iko wazi kuwa msanii Diamond Platnumz na Ommy Dimpoz wana ‘bifu’, lakini siku zote yapo mambo yanayoweza kuwafanya wapinzani wa jadi katika muziki kuwa kitu kimoja.
Ndivyo ilivyotokea baada ya Diamond kumpa pole Dimpoz ambaye kwa sasa amelazwa hospitali katika chumba cha uangalizi maalum (ICU).
Baada ya kuzagaa kwa taarifa kuwa Dimpoz hali yake kiafya si nzuri, Diamond ameweka picha ya msanii mwenzake huyo katika mtandao wake wa kijamii wa Instagram, akimwombea apone haraka na kurejea katika muziki.
“Inshaallah! Mwenyezi Mungu akufanyie wepesi uweze kupona haraka na kurudi kuendelea na sanaa ili pamoja tuzidi kupeleka muziki wetu mbali zaidi,” ameandika Diamond.
Hii ni mara ya kwanza kwa mwanamuziki huyu kuweka ujumbe katika mtandao wake kuhusu Ommy Dimpoz tangu walipojibizana katika vyombo vya habari Agosti, 2017 huku kila mmoja akimtuhumu mwenzake mambo mbalimbali.
Dimpoz akiwa msanii chini ya lebo ya Rock Star 4000 pamoja na Alikiba, wamekuwa na uhasama wa kimuziki na Diamond Platnumz kwa muda mrefu.
Mashabiki wa Diamond wamempongeza kwa kuweka pembeni tofauti zao za kibiashara na kumpa pole mwenzake kupitia mtandao huo wa kijamii.
Mmoja wa mashabiki hao precious.gal amesema, “hapo umeonyesha upekee Diamond siku zote usilipize kisasi kwa adui yako bali muombee mema, big up to you chibu.”
Naye herji_miney ameandika, “Sijutii kuwa shabiki wako. Unatupa muziki mzuri na hata nje ya muziki wako kuna vitu vya kujifunza.”