By Saddam SadickKATIKA kile kinachoonekana kama maboresho kwenye tuzo za dansi nchini, wanamuziki wamepewa fursa ya kutuma na kupendekeza kazi zitakazoshindanishwa.
Tuzo za Cheza Kidansi mwaka huu zinatarajia kufanyika Desemba, ambapo mwaka huu zinatarajia kufanyika jijini Dodoma kwa kushirikisha zaidi ya kazi 50 kutoka kwa wasanii mbalimbali.
Mkurugenzi wa Cheza Kidansi Entertainment, Bernard James, amesema mwaka jana mapendekezo yalifanywa na jopo la wataalamu wa muziki nchini, hivyo mwaka huu wasanii ndio watapendekeza.
Bernard amesema wanamuziki binafsi na wale walio kwenye bendi watatuma majina na taarifa sahihi ya kazi zao zitakazoshindanishwa katika vipengele mbalimbali.
''Haya ni maboresho makubwa ili kuondoa lawama na malalamiko yasiyo na tija mfano katika wimbo bora, bendi au mwanamuziki atatuma kazi zake zilizotoka mwaka huu kwa waandaaji ili kuziingiza katika mchakato kabla ya kupigiwa kura,'' amesema Bernard
Ameongeza kuwa wameamua kufuata mfumo wa tuzo mbalimbali zilizowahi kutolewa nchini katika tasnia tofauti ili kunogesha zoezi hilo mwaka huu na kuwaomba washiriki kuzingatia utaratibu uliowekwa na waandaaji.