Siku moja baada ya uongozi wa Simba kuomba radhi kwa waumini wa dini ya Kikristo na viongozi mbalimbali wa dini wasanii Tunda Man, Stan Bakora na Abdul Kiba nao wameibuka na kuomba radhi.
Wasanii hao kwa pamoja, Agosti 8, 2022 waliingia Uwanja wa Taifa, jijini Dar wakiwa na jeneza pamoja na msalaba wakiwa na lengo la kuwatania watani wao Yanga SC katika shoo yao lakini jambo hilo likazua tafran kuwa limeidhihaki dini ya Kikristo.
“Lengo letu lilikuwa ni kuwatania watani wetu lakini tumeona baadhi ya viongozi wa dini na watu wengine hususan Wakristo hawakupendezwa na ule ubunifu wetu hivyo tunaomba radhi sana, watusamehe,” alisema Tunda.
Kwa upande wake Stan Bakora naye aliungana na Tunda kwa kusema, wanaomba radhi walikosea na kama vijana ambao wanategemea sanaa kama kazi yao, wawasamehe.
“Kama maandiko yanavyosema samehe saba mara sabini, tunaomba nasi watusamehe. Lengo letu lilikuwa kumkera mtani na kama mlivyoona walikereka sana hususan katika ile risala ya wasifu wa marehemu,” alisema Stan huku Abdu Kiba naye akimuunga mkono.