Dar es Salaam. Kundi la muziki wa kizazi kipya nchini Tanzania, The Mafik limepaniwa kuweka historia kwenye tamasha la busara litakalofanyika hivi karibuni kisiwani Zanzibar.
Wasanii wa kundi hilo Hamadi Hassan maarufu Hamadia na Salehe Husseni ‘Rhino’ ni miongoni mwa watakaotumbuiza kwenye tamasha hilo linalofanyika kila mwaka.
Wakizungumza katika mahojiano na Mwananchi wasanii hao wamesema ni heshima kupata nafasi hiyo ambayo wamebainisha kuwa wataitendea haki.
"Baada ya tamasha habari ya mjini itakuwa ni The Mafik. Ni heshima kubwa kwetu kwa sababu wanamuziki wengi wanatafuta nafasi hiyo bila mafanikio,” amesema Hamadia.
Ameongeza, “huwezi kuitwa kutumbuiza kwenye tamasha hilo kama huwezi kuimba vyema jukwaani huku ukipigiwa vyombo. Kupata fursa hiyo kunaonyesha ni namna gani ambavyo tunakubalika katika eneo hilo la kuburudisha mashabiki.”
Rhino amesema tayari wameanza maandalizi kuelekea kwenye tamasha hilo "tamasha litakuwa na watu zaidi ya 20,000 kutoka nje ya Tanzania,itakuwa nafasi nzuri kwetu na namna tunavyojiandaa nia ni kuhakikisha baada ya tamasha The Mafik ndiyo iwe habari ya mjini.”