MAMLAKA ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imesema ziara ya msanii wa muziki wa kizazi kipya, Faustina Mfinanga maarufu kwa jina la Nandy katika Bandari ya Kigoma itaongeza fursa ya kuitangaza bandari hiyo hivyo kuongeza shehena ya mizigo bandarini hapo.
Meneja Uhusiano na Mawasiliano wa TPA, Nicodemus Mushi alisema hayo jana wakati wa ziara ya Nandy katika bandari hiyo.
Mushi alisema Nandy ni msanii maarufu ndani na nje ya Tanzania hivyo kwenda kwake hapo kutasaidia kuitangaza TPA na shughuli zake.
Meneja wa Bandari ya Kigoma, Augustino Nyoni, alisema kumekuwa na ongezeko la shehena kuingia na kutoka kupitia bandari hiyo na kwamba, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) inapitisha asilimia 75 ya mizigo yake katika bandari hiyo.
Wakati akiwa bandarini hapo, Nandy alisema atatumia nafasi yake kutangaza faida za kuitumia Bandari ya Kigoma kusafirisha mizigo.