MWIGIZAJI wa filamu nchini, Steven Mengele ‘Steve Nyerere’ ambaye ni mwanachama wa CCM, ameahidi kuendelea kupambana kwa ajili ya chama hicho, licha ya kushindwa kura za maoni katika Jimbo la Iringa Mjini.
Steve alipata kura sita na kushika nafasi ya tisa katika wagombea 57 waliokuwa wakiwania kuteuliwa kugombea ubungo wa Iringa Mjini. Mshindi wa kura za maoni alitangazwa kuwa ni Jesca Msambatavangu.
Akitoa ufafanuzi baada ya matokeo hayo jana, Steve alisema amepokea matokeo hayo kwa moyo wa dhati na kumshukuru Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Ali Hapi kwa kumuunga mkono mpaka kufikia hatua hiyo.
“Asante chama changu, viongozi wote wa CCM, wakiongozwa na Ali Hapi, na wanachama wote wa chama hiki kukosa kura sio sababu ya kuacha mapambano,” alisema Steve Nyerere.
Wasanii wengine ambao walionesha nia ya kugombea kwenye majimbo tofauti na kushindwa kwenye kura za maoni kupitia CCM, ni Emmanuel Mathias ‘MC Pilipili’ ambaye hakupata kura Jimbo la Bahi, Silvery Mujuni ‘Mpoki’ Jimbo la Kigamboni hakupata kura yoyote na Zamaradi Mketema aliyepata kura mbili katika jimbo la Kinondoni.