Dar es Salaam. Imeelezwa pamoja na sauti nzuri, kipaji, nidhamu ndiyo siri ya mafanikio ya wasanii.
Hayo yamesemwa leo Jumanne Septemba 24,2019 na Katibu wa kundi la taarabu asili liitwalo Taifa Zanzibar, Taimuri Rukuni alipokuwa akifanya mahojiano na MCL Digital, kwenye Tamasha la Utamaduni Afrika Mashariki (Jamafest) linaloendelea jijini Dar es Salaam.
Rukuni amesema hayo wakati wakijiandaa kupanda jukwaani kutoa burudani usiku wa leo Jumanne ikiwa ni utekelezaji wa ratiba ya tamasha hilo.
Amesema wao nidhamu inaanza, vingine ikiwamo kipaji halisi vinafuatia na ndiyo maana wamenoa wasanii wengi wakongwe wanaoendelea kufanya vizuri kwenye muziki huo.
“Waimbaji mahiri na makini kama Bi Kidude, Nasma Khamis ‘Kidogo’, Fatuma Dogodogo ambao ni marehemu kwa sasa.”
“Wengine ni Bi Mwanahawa Ally, Mzee Yusuf, Khadija Kopa, Sihaba Juma, Muchacho, Othuman Sudi, Rukia Ramadhani na Khadija Yusuf”, hao ni mfano na wameendelea kufanya vizuri na nidhamu wanazeeka nayo, ”amesema.
Pia Soma
- DC Dodoma atangaza operesheni kuwasaka vibaka
- Simba, Nyati wapagawisha washiriki tamasha la Jamafest
- Tanzania kupewa uenyeji Jamafest 2032
- Vijiji 165 Tanzania kupata neema ya maji kutoka Benki ya Dunia
Nyimbo kali za kundi hilo ni pamoja na ‘Mazoea yana taabu’ ‘Njoo mpenzi’ na ‘Ya laiti’.
Amesema tofauti na makundi mengine ya taarabu wao wamefanikiwa kutokana na kuiheshimu asili ya muziki huo.
“Pamoja na mambo mengine taarabu ni umaridadi, kuipenda kazi, kuficha tungo na kujisitiri.”
“Hivyo kwa sifa hizo na nyingine lazima mwimbaji anayepita hapa awe mzuri anayejua kutunga na kuimba na staha pia, hao niliowataja wanafanya vizuri kwenye muziki licha ya kuhamia kwenye modern taarabu,” amejinasibu Rukuni.
Amesema kutokana na nidhamu waliyojengewa waimbaji wote waliopita kwenye kundi hilo wanaliheshimu hadi leo na kukiwa na jambo wanahitajika hurudi wote na kujumuika na wenzao.
Tamasha la Utamaduni la Afrika Mashariki (Jamafest) lilianza Septemba 21, 2019 litafikia kilele Septemba 28, 2019, likizikutanisha pamoja nchi sita zinazounda Jumuia ya Afrika Mashariki.