MSANII wa muziki wa kizazi kipya, Karen Gadner ‘Malkia Karen’ amesema Zuwena Mohamed ‘Shilole’ ni kama Mama kwake kwani amemchangamsha katika muziki na biashara.
Akizungumza Dar es Salaam wakati akitambulisha wimbo wake mpya wa Kwetu, nyota huyo alisema Shilole amekuwa akimuamsha usingizini na kumtaka aamke kupambana kutimiza malengo yake.
“Shilole amenisaidia kuniamsha ni mtu anayependa kupambana, anataka kukuona na wewe unafikia ndoto zako, mara nyingi amekuwa akiniambia amka, changamka usilale,” alisema.
Alisema hata biashara aliyowahi kuanzisha ya kuuza juisi ya miwa ni kutokana na hamasa kubwa kutoka kwa msanii huyo mkongwe.
Nyota huyo ametambulisha wimbo wake huo akiwa ameshirikiana na mkongwe Judith Wambura ‘Lady Jaydee’ na kuomba kuungwa mkono katika kazi yake hiyo.
Karen ambaye ni mtoto wa mtangazaji maarufu wa kituo cha radio cha Clouds, Gadner Habash licha ya kutoa nyimbo kadhaa bado jina lake halijavuma ila ana sauti ya kumtoa nyoka pangoni, akisema anajaribu kufuata nyayo za aliyewahi kuwa mama yake wa kufikia, Lady Jaydee.
Lady Jaydee alisema msanii huyo alianza kuimba muziki tangu akiwa anasoma shule ya msingi ila alikuwa akimsisitizia kumaliza masomo kisha aendelee na sanaa hiyo na kwamba aliwahi kumtolea nyimbo kama tatu huko nyuma. Aliwaomba mashabiki wa muziki kumuunga mkono binti huyo ili atimize malengo yake.