Ashiraf Geuza maarufu' Uchebe' amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni akikabiliwa na kosa la kumjeruhi Zuwena Mohamed maarufu 'Shilole' na kumsababishia maumivu makali.
Akisoma hati ya mashtaka Wakili wa Serikali, Chesensi Gavyole mbele Hakimu Mkazi Hudi Hudi, alidai kuwa Julai 6, 2020 maeneo ya Dar Estate Kinondoni jijini Dar es Salaam mshtakiwa huyo alimpigia Zuwena Mohamed sehemu ya kichwa na shingoni na kumsababishia maumivu makali.
Hata hivyo mshtakiwa huyo alikana shtaka linalomkabili.
Gavyole alidai kuwa upelelezi umekamika na aliiomba mahakama hiyo ipange tarehe nyingine.
Hakimu Hudi alisema dhamana ipo wazi mshtakiwa anatakiwa awe na wadhamini wawili ambao wanatakiwa kuwa na barua inayotambulika na watasaini bondi ya Sh2 milioni pamoja na mshtakiwa
Mshtakiwa huyo alikidhi masharti ya dhamana shauri hilo limeahirishwa hadi Septemba 23, 2020 itakapokuja kwa ajili ya usikilizwaji wa hoja za awali.