Msanii wa maigizo Bongo ambaye amepata umaarufu kupitia Wimbo wa Mbosso wa Sele 'Selemani' amesema kuwa kutokana na hali yake duni ya kimaisha, aliyekuwa mchumba wake alimuacha.
Selemani ambaye anaishi mitaa ya Tandika amesema hayo ikiwa ni siku chache baada ya Mbosso kuachia video ya wimbo huo aliomshirikisha msanii Chley kutoka nchini Afrika Kusini.
"Kwa sasa sina mpango wa kuoa kwa sababu mchumba wangu alikimbia kisa sina kipato. Niliwahi kumpa Tsh 50,000 akafungua genge lakini baadae kipato changu kiliposhuka akaamua kuniacha.
"Aliniambia hawezi kuwa na mwanaume ambaye hana pesa, nilimuelewa kwa sababu mimi ni mwanaume. Lile genge lilikuwa likifanya vizuri, alikuwa anauza sana lakini baada ya kuondoka kwangu hata lile genge lilikufa. Kwa sasa sitaki kuoa kwanza mpaka nitafute pesa kwanza," amesema Sele.