Dar es Salaam. Msanii wa filamu nchini Tanzania, Rose Ndauka na wa Bongofleva, Harmorapa ni kati ya wasanii watakaokuwa mabalozi katika kutangaza utalii wa mikoa ya Kusini.
Hayo yamebainika leo Jumatatu Septemba 16, 2019 katika mkutano kati ya balozi wa utalii nchini Tanzania, Nangasu Warema na waandishi uliolenga kuzungumzia maonyesho ya utalii wa Kusini yatakayofanyika mkoani Lindi Septemba 20 hadi 22,2019.
Nangasu amesema Rose Ndauka, Harmorapa ambaye jina lake halisi ni Athumani Omar, Mkali Wenu na Miss Tanzania 2018, Queen Elizabeth Makune ni miongoni mwa watu watakaofanya nao kazi katika kutangaza utalii wa Kusini.
"Watu wengi hawajui kama Kusini mwa Tanzania nako kuna vivutio vingi vya utalii, naamini kupitia wasanii hawa tutashirikiana katika kuvitangaza na watu kwenda kutembelea," amesema.
Rose Ndauka amesema kupitia ubalozi aliopewa anaamini atayajua mengi ya kuwafahamisha watu kuhusu utalii uliopo Kusini.
"Nasikia kuna kivutio kinaitwa Bustani ya Mungu kuna maua yanaota bila kumwagiliwa wala kuwekewa mbolea na vingine vingi ambavyo nikivijua vyema nitakuwa balozi mzuri kwa watu wengine kuelezea uzuri wake," amesema.
Pia Soma
- Mradi wa kukusanya takwimu za samaki Bahari ya Hindi waanza
- VIDEO: Mama adaiwa kumkata shingo mwanaye
- Euro 44 bilioni kuwekeza miradi nchi kumi za Afrika
Ameomba watu wasisite kwenda kuwekeza biashara mbalimbali.