Dar es Salaam. Romy Jones, binamu wa mwanamuziki Naseeb Abdul maarufu Diamond Platnumz amezua gumzo katika mitandao ya kijamii baada ya kumpongeza ndugu yake ya kupata mtoto wa tano.
Gumzo hilo limetokana na mashabiki wengi wa mwanamuziki huyo kudai kuwa ana watoto wanne na si watano kama alivyoeleza Jones.
Jones ameandika jambo katika ukurasa wa mtandao wa kijamii wa Instagram akimpongeza Diamond baada ya jana Jumatano Oktoba 2, 2019 mpenzi wa mwanamuziki huyo, Tanasha Donna kujifungua mtoto wa kiume.
Diamond anayemiliki tuzo zaidi ya 35 alifurahia kuzaliwa kwa mwanaye huyo wakati akisherehekea siku yake ya kuzaliwa.
Wakati Diamond akipongezwa kwa kuwa na watoto wanne, Jones amesema ndugu yake ni baba wa watoto watano.
“Hongera sana kwa kupata mtoto wa kiume kwenye siku yako ya kuzaliwa! Hakika huyo ndio atakua pacha wako, Allah akutunzie, akulindie na akukuzie pia Inshaallah panapo maajaliwa na mimi nitapata japo mmoja wa kukuita wewe baba.”
Pia Soma
- Tundu Lissu aingia mkataba na kampuni ya kimataifa kulinda haki zake
- VIDEO: TRA yataja siri ya kuvunja rekodi makusanyo Septemba
- Kukatika umeme Dar kwaondoka na mfanyakazi Tanesco
Zulfa Mohammed aliandika, “Hivi ni watano kumbe.” Huku Jenifer akisema, “kuna mtu anaweza kunisaidia kunielewesha hao watano huyo mmoja sijawahi kumsikia, kumbe alikuwa na watoto wanne?”
Kupitia ukurasa wake katika mtandao wa Twitter, Diamond ameandika “07:28 mchana wa Oktoba 2, 2019 kisha akaweka alama mbili za kopa na katikati au rozi jekundu.”
Mashabiki wa nyota huyo wametoa pongezi zao kupitia mtandao wa Instagram ikiwemo ukurasa rasmi wa redio ya Wasafi (WasafiFm) ambayo Diamond ni mkurugenzi wake.
“@DiamondPlatnumz na @Tanashadonna wamefanikiwa kupata mtoto wa kiume siku ya leo…Huyu ni Mtoto wa kwanza wa Tanasha na wa nne kwa upande wa Diamond, andika chochote kuwapongeza @Diamondolplatnumz na @Tanashadonna kwa kupata Mtoto,” ujumbe ulisomeka hivyo.
Dada wa Diamond Esma ameandika, “Ooops hongereni kwa Baby Boy ila na hongera na mimi najipongeza Aunty sio kwa zoezi lile mwanangu umenikomesha sio kwa kunifanya niwe macho mpaka sasa hivi.”