Nyimbo za Wanamuziki wa Kitanzania zinatarajiwa kuanza kupigwa kwa asilimia 100 kwenye viwanja vya ndege hapa nchini ili kuendelea kuutangaza muziki wa kitanzania.
Makubaliano hayo yamefikiwa baada ya kikao cha Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamis Mwinjuma ambaye amekutana na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini katika kikao kilichofanyika Jijini Dar es salaam.
Katika kikao kazi hicho, Naibu Waziri Mwinjuma ametoa rai kupitia kwa Mkurugenzi wa Mamlaka hiyo Musa Mbura kufanya hivyo ili kutangaza muziki wa kitanzania kwa wageni wanaoingia na kutoka nchini.
Kikao hicho kimehudhuriwa na Mkurugenzi wa Maendeleo ya Sanaa, Dkt. Emmanuel Ishengoma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa la Taifa, (BASATA) Dkt. Kedmon Mapana, Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu, Dkt. Kiago Kilonzo na Kaimu Mtendaji Mkuu wa COSOTA, Baraka Katemba.