MSANII mkongwe wa muziki wa dansi nchini Nguza Viking ‘Babu Seya’ amesema mshtuko mkubwa aliopata kufuatia kifo cha Rais wa awamu ya tano John Magufuli pengine watu wangesikia na yeye amefariki.
Babu Seya ni miongoni mwa wafungwa waliookolewa na Magufuli kutoka kwenye kifungo cha maisha jela na mtoto wake Papii Kocha na kuachwa kuwa huru Desemba mwaka 2017.
Akizunguza Dar es Salaam jana, nyota huyo alisema “baada ya mtoto wangu kunipigia simu kunipa taarifa za msiba wa Rais Magufuli nilipata mshtuko mngenisikia na mimi nimeondoka.”
Alisema taarifa hizo zilisababisha yeye kukosa usingizi akitafakari matendo mema aliyomfanyia rais huyo enzi za uhai wake.
Nyota huyo aliwahimiza watanzania kutoogopa juu ya kilichotokea akiamini bado kiongozi yupo nao kiroho.
Magufuli alifariki dunia Jumatano ya wiki hii kutokana na tatizo la moyo.