MWISHONI mwa mwaka 2018, Diamond Platinumz alikuwa matatani baada ya wimbo wake wa Mwanza Nyegezi alioshirikiana na Rayvanny kupigwa marufuku na Basata kwa kukosa maadili katika maudhui yake.
Diamond Platinumz ambaye wakati huo alikuwa kwenye ziara zake za kimuziki za Wasafi Festival aliupiga wimbo huo alipokuwa ziarani Mwanza, na ‘so’ kuwa kubwa zaidi.
Basata wakajihisi kudharauliwa na kumshushia rungu kubwa kwa kumfungia kufanya matamasha ndani na nje ya nchi.
Wakati rungu hilo lilishuka, tayari alikuwa anajiandaa na mfululizo wa matamasha makubwa nchini Kenya.
Lakini baadaye busara zikatumika, matamasha ya Kenya yakafanyika...maisha yakaendelea.
Diamond mwenyewe aliandika waraka mrefu kwenye moja ya akaunti zake za mitandao ya kijamii kutetea wimbo kwa kusema jina la wimbo huo limetafsiriwa vibaya kwa sababu Nyegezi ni sehemu ya mkoa wa Mwanza hapa nchini.