Burudani

Habari

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Ndugu wavutana mazishi ya Jengua

91607625c08cb057362f4e9e6e2a9ac0.jpeg Ndugu wavutana mazishi ya Jengua

Thu, 17 Dec 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MWILI wa mwigizaji wa filamu nchini, Mohamed Fungafunga ‘Jengua’ umezikwa jana katika makaburi ya Mburahati kwa Jongo Dar es Salaam karibu na nyumbani kwao, huku kukiibuka utata kutoka kwa wanafamilia.

Jengua alifariki dunia juzi Mkuranga baada ya kusumbuliwa na ugonjwa wa kiharusi kwa muda mrefu.

Katika mazishi hayo familia yake ilikuwa ikivutana juu ya wapi akazikwe, lakini baada ya mazungumzo na kupata muafaka waliamua kwenda kumzika Mburahati ilikokuwa imepangwa tangu awali baada ya kutokea kwa kifo chake.

“Tumegundua haina haja ya kuendelea kuzozona ni wapi akazikwe tukaona ni bora Mburahati lakini na sisi huku Mkuranga tutaweka msiba sababu ndipo alipokuwa mkewe na anapokaa eda,” alisema mmoja wa ndugu ambaye hakutaka jina lake litajwe.

Kwa mujibu wa familia yake, Jengua alikuwa akiishi nyumbani kwao Mburahati alikokuwa anafanya shughuli zake za sanaa kwa muda mrefu ndio maana walipendekeza azikwe huko ila mke wake na mtoto walitaka akazikwe Mkuranga.

Hata hivyo baadaye waliafikiana na kuamua azikwe Mburahati ili mambo mengine yaendelee kama yalivyopangwa.

Mazishi hayo yalihudhuriwa na watu wengi wakiwemo wasanii mbalimbali kama Fresh Jumbe, Aziz Kimindu ‘Nyapinyapi’, Lucas Lazaro ‘Joti’, Jacob Stephan, Vicent Kigosi, Single Mtambalike, Steve Nyerere, Fatma Makongoro na watu wengine maarufu.

Chanzo: habarileo.co.tz