NYOTA wa muziki wa Bongo Fleva, Emmanuel Elibariki ‘Nay wa Mitego’, amesema amegundua kwamba mashabiki wengi wa muziki wake ni viongozi wa Serikali na wanasiasa.
Akizungumza na gazeti hili msanii huyo anayetamba na wimbo wake mpya alioupa jina la ‘Mama’, alisema hiyo imemsaidia kupata watazamaji wengi kwenye mtandao wake wa You Tube.
“Nafurahi kuona muziki wangu unasikilizwa na kufuatiliwa sana na watu wazito wanasiasa nadhani nikutokana na ujumbe uliopo ndani yake na hii inanipa nguvu sana katika kazi zangu za muziki,” alisema Nay wa Mitego.
Msanii huyo alisema wasanii wenzake wengi wa Tanzania wameegemea zaidi kuimba mapenzi wakati kuna mambo mengi zaidi ambayo yanaweza kumfanya msanii kuwa juu na maarufu zaidi.
Nay wa Mitego alisema kwa mtazamo wake muziki unalipa sana na kuthibitisha hilo ndio maana wasanii wengi wamebadilisha sana maisha yao, lakini hiyo inategemea na juhudi ya msanii mwenyewe na aina ya muziki anaoimba.
Mkali huyo asilimia kubwa ya nyimbo zake ni zile ambazo zinaisifu au kuielimisha Serikali juu ya jambo fulani, jambo ambalo limekuwa likiwafanya wanasiasa kuzifUatilia kwa karibu kazi zake.