MSANII wa muziki wa kizazi kipya, Juma Mussa ‘Jux’, amesema akimpata mpenzi mpya atamsahau mpenzi wake wa zamani.
Jux ambaye alikuwa kwenye uhusiano wa muda mrefu na Vanessa Mdee, anaonekana kuteswa na penzi hilo la zamani.
Vanessa baada ya kuchana na Jux takribani miaka mitatu iliyopita, aliingia kwenye uhusiano na Rotimi raia wa Nigeria na kwasasa ni mjamzito na wanatarajia kupata mtoto hivi karibuni.
“Nikimpata mpenzi mpya basi itakuwa njia ya mimi kumsahau mtu ambaye nilikuwa naye kwenye mahusiano,” alisema.
Jux hivi karibuni alitoa wimbo unaoitwa ‘Sina neno’ maalumu kwa Vanessa akimtakia kila la heri na kusema hana chuki na yeye.
Wawili hao walikuwa wapenzi wa muda mrefu kabla ya kuachana na kurejeana tena lakini hawakukaa muda mrefu kabla ya kila mmoja kushika njia yake.
Kwenye mahojiano waliyofanya kwa nyakati tofauti, walisema kwamba hawakuachana kwa ubaya bali waliamua kila mmoja aendelee na maisha yake maana kwa hali waliyofikia wasingeweza tena kuwa wapenzi.