Dar es Salaam. Msanii Hawa Said maarufu ‘Hawa Nitarejea’ amesema hasisimuliwi na wanaume tena baada ya mwili wake kufa ganzi, kutokana na vitendo alivyotendewa.
Amesema anamshangaa mwanaume aliyemsababishia matatizo kiasi cha kuwa mlevi aliyepitiliza kuanza kumtumia ujumbe mfupi baada ya kupona na kutoa wimbo.
“Namshangaa kwa sababu mwili wangu umekufa ganzi, nimepitia mambo mengi sana kuhusiana na wanaume akiwamo yeye,” amesema Hawa.
Hawa ameyazungumza hayo leo Alhamisi Agosti 15, 2019, alipotembelea ofisi za Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) ambayo ni wazalishaji wa magazeti ya Mwananchi, The Citizen, Mwanaspoti pamoja na mitandao ya kijamii.
Amesema mwanaume huyo (hakuwa tayari kumtaja jina) alimrubuni kwa mapenzi akambadili dini na kufunga naye ndoa ya kanisani.
“Kitendo cha yeye kunibadili dini kiliwaudhi sana familia yangu na ndugu zangu, lakini kwa kuwa nilikuwa nimependa sikujali jambo lililosababisha wanitenge na hata nilipokuwa kwenye unywaji pombe hakuna aliyekuwa tayari kunisaidia kwa kile walichodai kuwa nilijitakia mwenyewe.”
Pia Soma
- Rais wa Shelisheli atua Tanzania kushiriki mkutano wa SADC
- TRA yawalima barua wamiliki migodi ya Tanzanite
- Mifuko ya plastiki yabainika K’koo, Waziri Simbachawene atoa maagizo
- Meya Kinondoni aelezea jinsi Coco Beach itakavyoboreshwa
Amesema ameishi kwenye mateso ya ulevi kupita kiasi na kupata maradhi ya moyo, “Namshukuru sana Diamond, kuguswa na ugonjwa wangu na kunitibia, sitaki kurudi tena huko.”
“Nilishangaa siku moja nilipoweka wimbo Instagram akanijia DM na kuniuliza ‘nyie hamjambo huko’ sijamjibu kwa sababu sitaki heka heka zake wala za mwanaume mwingine,” amesema
Amesema kwa sasa anaelekeza akili zake kwenye muziki na biashara.