Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamisi Mwinjuma ‘Mwana FA’ amesema kuwa ataomba mwongozo Serikalini iwapo anaruhusiwa kuendelea kufanya kazi za muziki licha ya kuwa naibu waziri.
Mwana FA amesema hayo wakati akihojiwa baada ya kuwasili katika makao makuu ya wizara hiyo na kukabidhiwa ofisi.
“Kinachoniuma ni nyimbo zangu nilizonazo ndani, sasa sijui utaratibu utaniruhusu kuzitoa au vipi? Mimi mwenyewe sijawahi kuona duniani kote Waziri akitoa wimbo.
“Lakini nyimbo ninazo, tiutaomba mwongozo tuone kama inaruhusiwa kama inaruhusiwa basi hakuna kitu kitakachopungua, mizingo itaendelea kudondoka.
“Mimi sio waziri wa katiba na sheria, mimi ni naibu waziri wa Sanaa na michezo, kwa hiyo pengine nitatakiwa kuonyesha mifano kwa sababu Naibu waziri anaruhusiwa kwenda kucheza mpira iweje muziki azuiwe? Ngoma zipo, tukiruhusiwa tutaziachia,” amesema Mwana FA.