Hadija Kanyama wa Tanzania ameibuka mshindi katika mashindano ya Miss Kiziwi Dunia 2022 huku kwa upande wa Mr Kiziwi, ushindi umeenda kwa Gareth Kelaart, mshiriki kutoka nchini Australia.
Mashindano hayo yalifanyika katika ukumbi wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es salaam usiku wa kuamkia leo Jumapili Oktoba 30, 2022.
Dalili za Hadija kutwaa taji hilo, zilionekana tangu alivyokuwa akipita kwa mikogo jukwaani na kuufanya umati wa watu waliofurika katika ukumbi huo kulipuka kwa shangwe.
Hadija ameibuka mshindi akiwabwaga wenzake 12 kutoka mataifa mbalimbali.
Ukiacha kuwa Miss Dunia, Hadija pia alishinda kipengele cha Miss katika kucheza muziki wa asili.
Mashindano hayo pia hayakuwaacha nyuma wamama ambapo ushindi ulienda kwa mwanamama kutoka nchi ya Australia na kufanya Australia kuondoka na ushindi wa mataji mawili katika fainali hizo.
Faininali za mashindano hayo zilizoanza saa mbili usiku na kumalizika saa nane usiku, kwa washiriki kupita na mavazi mbalimbali ikiwemo la ufukweni, utamaduni, ubunifu na la usiku.
Mgeni rasmi katika fainali hizo alikuwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na makundi maalum, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Dk Doroth Gwajima huku mgeni maalumu akiwa Waziri wa Sanaa, Utamaduni na Michezo, Mohamed Mchengerwa.