Dar es Salaam. Waandaaji wa shindano la kumsaka Miss Tanzania, wamesema mshindi wa shindano hilo hapatikani jukwaani siku ya fainali kama watu wanavyodhani.
Hayo yamesemwa leo Alhamisi Agosti 29,2019 na Mkurugenzi wa kampuni ya ‘The Look’, Basila Mwanukuzi ambao ndio waandaaji wa shindano hilo kuanzia mwaka 2018, alipofanya ziara katika ofisi za Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) inayozalisha magazeti ya Mwananchi, The Citizen, Mwanaspoti zilizopo Tabata relini, Dar es Salaam nchini Tanzania.
Katika ziara hiyo, Basila ameambatana na Miss Tanzania 2019, Sylivia Sebastian, mshindi wa shindano hilo aliyeshika namba nne, Gratness Nkuba namba tatu, Queen Magese.
Amesema uchaguzi wa kumpata mrembo atakayeiwakilisha nchi katika shindano la Miss World huanzia kambini.
“Wakiwa kambini, hufanyiwa ‘pre judge’ ambapo majaji wa shindano wanahakikisha warembo hao wanakuwa na sifa ambazo zinatakiwa Miss World ikiwemo suala la umbo, uzuri namna ya kujieleza na mengineyo.”
“Hivyo mpaka anapanda jukwaani siku ya mwisho asilimia 60 majaji wanakuwa wameshafanya yao na arobaini iliyobaki ndio inamalizikia siku ya fainali jukwaani,” amesema
Pia Soma
- Walimu 30,000 wafukuzwa kazi Uganda
- Ajiua, amjeruhi mkewe na kuacha ujumbe wa kumuomba radhi Rais Magufuli
- Agizo la Makonda kwa watendaji wa mitaa Dar
“Watu huwa wanalichukulia poa suala hilo, sisi tumelipa umuhimu kuwa pamoja na mambo mengine warembo wajue kuna Mungu na waishi kwa kumtumainia, ”amesema Basila.
Shindano la Miss Tanzania lilifanyika Agosti 23, 2019 Jijini Dar es Salaam, ambapo Silvia Sebastian mwakilishi kutoka Kanda ya Ziwa alitwaa taji hilo na kuondoka na kitita cha Sh10 milioni.