MKURUGENZI na muanzilishi wa lebo ya Next Level, Raymond Mwakyusa ‘Rayvanny’, amemtambulisha msanii Macvoice ambaye anakuwa msanii wa kwanza kusainiwa na mkali huyo wa bongofleva tangu alipozindua lebo yake mwaka huu.
Rayvanny ambaye anafanya kazi chini ya lebo ya Wasafi inayomilikiwa na msanii Diamond Platnumz, naye ameanza kuwashika mkono wasanii wengine ili watimize ndoto zao kama ilivyokuwa kwake alipoibuliwa na Hamadi Ally ‘Madee’.
Akizungumza na gazeti hili jana, Rayvanny alisema anafuraha kumtangaza msanii wa kwanza katika lebo yake kwani ni hatua kubwa kwake na anaamini msanii huyo atafika mbali iwapo hataridhika mapema.
“Muda mrefu nilikuwa naulizwa maswali ni lini nitaanza kusaini wasanii katika lebo yangu ya Next Level, nimeanza na Macvoice ambaye naamini mtampokea ni kijana mwenye kipaji kikubwa cha kuimba na kuandika mashairi. Leo nataka niwaambie kuwa Macvoice ni mwanafamilia wa Next Level, ila atatambulishwa rasmi Ijumaa tarehe 24, karibu katika familia kubwa ya muziki Macvoice,” alisema Rayvan.