Akizungumza mke wa marehemu, Saada Nyambibo ameeleza kauli ya mwisho ya mume wake na amesema Malu alikuwa anaumwa karibu mwezi mmoja uliopita na walienda Hospitali ya Rabininsia na kugundulika na alikuwa na maambukizi kwenye damu na alianza dozi hadi kufika Pasaka alikuwa amemaliza na juzi Aprili 4 alifanya sherehe ya kumbukizi ya siku ya kuzaliwa kwake.
Saada amesema alipata taarifa kutoka kwa Patcho Mwamba kuwa mumewe amefariki dunia, lakini kabla ya taarifa hiyo, Malu alirudi nyumbani saa mbili usiku kisha kutoka muda huo kwenda kazini, ila baada ya saa tatu ndio akapata taarifa hiyo ya msiba wa nyota huyo mwenye asili ya DR Congo.
Kwa sasa msiba upo nyumbani kwa marehemu Salasala wakiendelea kusubiriwa ndugu wa marehemu wakitokea Lubumbashi, DR Congo na mwili ukiwa umehifadhiwa Hospitali ya Lugalo.
Saada amesema yeye na Malu walifunga ndoa tangu Juni, 2004 na wamebahatika kupata watoto wanne.