MSANII wa kizazi kipya Omary Mwanga ‘Marioo’ amesema kuishi maisha ya kawaida ni moja ya sababu inayomfanya kuendelea kutunga nyimbo zinazowavutia mashabiki wake.
Akizungumza Dar es Salaam juzi, Marioo anayetamba na nyimbo kadhaa ikiwemo Inatosha alisema kuridhika na anachokipata kwa nguvu zake na kuongeza juhudi ya kutafuta ni utamaduni wake.
“Siku zote mafanikio yanakuja kwa wakati ambao Mungu kapanga, nimechagua maisha ya kawaida kwa kudhibiti tamaa ndio maana naendelea kutengeneza kazi nzuri na bora ambazo mashabiki wangu wanaziunga mkono,”alisema Marioo.
Alisema anafanya kazi ngumu na anapumzika muda mchache na mipango na malengo yake ni kuendelea kulinda hadhi anayopewa na mashabiki wake kwani wamekuwa wakimpandisha thamani kwenye soko la sanaa.
Alisema maandalizi ya kazi mpya yanaendelea hadi sasa ameshuti video mbili na wakati ukiwadia mashabiki wataona kupitia mitandao yake ya kijamii na kwenye vyombo vya habari.