MASHABIKI wa Simba wameonesha mapenzi ya dhati kwa timu yao baada ya kufika uwanjani leo kwenye tamasha la Simba Day na kuujaza Uwanja wa Benjamin Mkapa mapema.
Hadi kufika saa 8:15 mchana tayari majukwaa yote ya uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua watu 60,000 yalikuwa yamejaa mashabiki waliovalia jezi za Simba kwa wingi.
Sambamba na kujaza Uwanja, pia tiketi zote za kuingia uwanjani hapo leo zimeuzwa na kuisha kabla ya saa nane mchana kwa mujibu wa klabu hiyo.
Hata hivyo nje ya uwanja huo bado kuna nyomi la watu ambao wamepanga foleni kwenye mageti wakisubiri kuingia ndani huku wengine wakiburudika kwa aina tofauti.