Dar es Salaam. Baada ya mwanaye kutangazwa mshindi na kukabidhiwa hundi ya Sh20 milioni, mama mzazi wa Yusuph Nizar ambaye ni mshindi wa Bongo Star Search msimu wa 11 amemuomba amnunulie simu janja.
Akizungumza na Mwananchi mara baada ya mwanaye kutangazwa mshindi, Maria Kiharusi, alisema wakati kijana wake anakwenda katika fainali za mashindano hayo hakuwa na mategemeo ya kuwa na ushindi.
“Hakuniahidi zawadi yoyote kwa sababu hakuwa na uhakika wa kushinda, kwa kuwa amefanikiwa natamani aninunulie simu janja yenye uwezo wa kutumia programu ya Whatsapp”alisema.
Alisema walisikia kijana wao anashiriki mashindano ya kuimba wakiwa nyumbani kwao Makambako mkoani Njombe, ikabidi wamuite na kumuhoji kulikoni anaacha kufuata kilichomleta Dar?
“Unajua alikuja huku kwa ajili ya kusomea shahada ya elimu katika chuo cha Mwalimu Nyerere Memorial Academy badala yake amejiingiza katika mambo ya muziki, huku familia yetu ya wachaMungu”alisema mama huyo huku akiwa na tabasamu pana na kuongeza.
“Alitujibu haendi kutenda dhambi, anakwenda kufanya muziki tu ili atangaze jina lake, lakini atasoma kama tulivyokubaliana na tumuombee.” alisema.