Kigoma. Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma imetengua hukumu ya kifungo cha mwaka mmoja na siku mbili alichohukumiwa diwani wa Mwanga (ACT-Wazalendo), Clayton Chipando maarufu Baba Levo iliyotolewa na mahakama ya Wilaya.
Leo Alhamisi Novemba 21, 2019, Jaji mfawidhi wa mahakama hiyo, Ilvin Mugeta amesema kifungo hicho kilikuwa batili. Kutokana na uamuzi huo Baba Levo ataendelea kutumikia kifungo cha miezi mitano jela.
Jaji Mugeta amesema katika hoja sita zilizowasilishwa mahakama hapo amezingatia hoja moja ya hukumu iliyotolewa na mahakama ya wilaya ya kifungo cha mwaka mmoja na siku mbili.
"Mahakama imetengua hukumu ya diwani huyu ya kifungo cha mwaka mmoja na siku mbili na kubaki na hukumu ya awali ya kifungo cha miezi mitano kama ilivyotolewa na mahakama ya Mwanzo, "amesema Jaji Mugeta.
Baba Levo alikata rufaa mara mbili, ya kwanza ilikuwa Agosti 2 , 2019 baada ya mahakama ya Mwanzo kumhukumu kifungo cha miezi mitano jela.
Septemba 10, 2019 mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ilimuhukumu kifungo cha mwaka mmoja na siku mbili lakini Oktoba Mosi, 2019 Baba Levo alikata rufaa kupinga hukumu hiyo.
Baba Levo ambaye pia ni msanii wa kizazi kipya alishtakiwa kwa kosa la shambulio la kumdhuru mwili askari wa usalama barabarani, tukio analodaiwa kulifanya Julai 15, 2019.