MISS Tanzania wa mwaka 2001, Millen Magese amesema mashindano hayo bado hayajapoteza mvuto, isipokuwa vizazi vya sasa ni tofauti na waliokuwa wanaingia kwenye kinyang’anyiro hicho kwa miaka ya nyuma.
Akizungumza Dar es Salaam juzi, Magese alisema Watanzania waache kufananisha mashindani hayo na yale yaliyokuwa yanafanyika miaka ya nyuma na kwamba wanatakiwa kujitokeza kuwaaunga mkono kiuchumi waandaaji kuboresha shindano hilo.
“Mashindano haya yanahitaji kuungwa mkono na wanajamii wote na kada mbalimbali ikiwemo waandaaji kuwawezesha kiuchumi sio kubaki nyuma na kuanza kuzungumza mashindano yamepoteza mvuto, ukiona jambo linabomoka na mtu aliyeanzisha anapoteza muelekeo na baaadae anainuka tena niwakati wa kujitoa na kumuunga mkono na watu watambue katika shindano hili anapatikana mrembo mmoja anayepata fursa ya kuiwakilisha nchi kimataifa.
Ni vibaya kwa mtu aliyeanzisha anaanguka na kusahau kabisa hivyo watu waache utamaduni wa kufananisha mashindano na miaka ya nyuma na kama watajitokeza kuunga mkono wanaweza kupata mamiss wazuri zaidi, ” alisema Magese.
Pia Magese alisema zamani mashindano hayo yalikuwa na mvuto kwani kulikuwa na shindano moja na viongozi walikuwa tofauti na wasasa na ndiyo maana lilikuwa maarufu.
Miss huyo anayeishi Marekani aliyazungumza hayo juzi kwenye maandalizi ya ujio wa tukio la Beauty Legacy linaloandaliwa na Jacqueline Mengi, ambamba na matukio mengine yahusuyo tasnia ya urembo nchini.