Burudani

Habari

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Lofa Ajuta Kumkaribisha Kidosho Jangili Nyumbani Kwake

0fgjhs7qrtidig8do Lofa Ajuta Kumkaribisha Kidosho Jangili Nyumbani Kwake

Thu, 25 Mar 2021 Chanzo: kiswahili.tuko.co.ke

Jamaa mmoja kutoka Mtaani Hurligham, Nairobi amezongwa na mawazo kufuatia uamuzi wake wa kualika mrembo nyumbani bila kujua alikuwa akimkaribisha shetani.

Duru zinaarifu kuwa jamaa alikutana na kidosho kwenye hafla moja jijini na baada ya kufahamiana na kubadilishana nambari za simu wakaahidiania kukutana baadaye.

Kwa mujibu wa Taifa Leo, jamaa alikosa usingizi baada ya kukutana na kidosho huyo kutokana na sura yake, ngozi nyororo na figa ya kuvutia.

“Jamani nakupenda sana. Njoo kwangu nikutambulishe kwa wenzagu ambao hunicheka wakinitania eti nitazeeka nikitafuta. Niambie siku utakayokuwa huru nijiandae kukukaribisha,” jamaa alimbembeleza mrembo.

“Wewe niambie nije lini, waishi na nani kwako?” mrembo alisema.

Inasemekana jamaa alimuarifu dada kuwa alikuwa akiishi pekee yake na kwamba hakuwa na ndugu wala mke.

“Aisee, na waishi mtaa gani? Wajua ipo mitaa ya Eastlands nisiyoweza kutua mguu wangu. Naogopa kuibiwa na pia kuibwa mie,” mrembo alisema huku akipasua kicheko.

“Siishi Eastlands kwa mahasla. Kwangu ni Hurligham. Sisi ni wale wachache tuliotajirisha landlords. Imagine kwa mwezi hulipa elfu sabini na tano,” jamaa alijigamba.

Kisura alimuahidi jamaa atamtembelea siku ya Jumamosi akimtaka ampe makaribisho mazuri atakapowasili.

Penyenye zinasema kuwa siku hiyo ilipofika mrembo alifika kwa jamaa ambaye alimpa makaribisho mazuri.

Alifurahishwa kuona nyumba ilivyopangwa kinadhifu huku ikiwa imejaa vyombo vya bei ghali.

Wawili hao waliketi na kupiga gumzo kwa muda kabla ya mrembo kumuarifu lofa kuwa alitaka kuondoka saa kumi na mbili jioni ilipofika.

“Samahani, ipo simu napigiwa sasa na wazazi wangu. Usijitaabishe kunisindikiza kwa gari lako. Nitachukua teksi pale kisha kesho asubuhi nitarudi. Nahitaji kuwa na muda mrefu nawe. Nimekupenda sana,” kisura alimuaga jamaa na kuondoka.

Usiku saa tano hivi, duru zinarifu kuwa mlango wa jamaa ulibishwa na pindi alipoifungua alilakiwa na mtutu wa bunduki.

“Ukijaribu kupiga kelele, bunduki hii hapa itakutuma ahera sasa hivi. Rudi nyuma,” sauti ya kike iliamuru.

Bila kusita, majangili hao waliruka chumbani mwake wakabeba redio, runinga, zulia, makabati mawili na makochi ghali wakaiacha nyumba ikiwa tupu.

Si hayo tu kwani majambazi hao walimuamuru atoe pesa zote alizokuwa nazo chumbani akabaki bila hata senti mfukoni.

“Wakati mwingine ukitafuita vichuna, kuwa macho maana nimerudi kukutia adabu,” kidosho alishusha maski na kumkabili jamaa.

Inaarifiwa kuwa jamaa hakupata lepe la usingizi usiku huo akiwaza ni vipi mrebo jangili alimfumba macho kiasi hicho.

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia [email protected] au WhatsaApp: 0732482690.

Chanzo: kiswahili.tuko.co.ke