Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limemkaribisha msanii wa Bongo Fleva, Mbwana Yusuf Kilungi 'Mbosso Khan' ili kupata maelekezo kwa namna Tuzo za TMA zilivyoratibiwa badala ya kulaumu kwenye mitandao ya kijamii kuhusu vipengele vya tuzo hizo.
Hayo yamesemwa na Mrisho Mtumwa ambaye ni Mratibu wa Tuzo za TMA - BASATA wakati akifafanua kufuatia malalamiko ya Mbosso kupitia ukurasa wake wa Instagram akishangaa kwa nini EP yake ya ‘Khan EP’ haijaingizwa kwenye EP bora ya mwaka.
"Sisi hatuna jinsi ya kupata kazi ya msanii nje ya mfumo, sasa changamoto hapa inatokea kwenye vitu viwili kuna management na msanii," amesema Mrisho Mtumwa.
Hata hivyo Mrisho amemkaribisha msanii huyo kufika katika ofisi za BASATA ili kufunguliwa akaunti na kuoneshwa mfumo mzima wa mchakato wa tuzo hizo.
"Kwa hiyo wapo wasanii wanasema hawakupeleka kazi zao ila wamependekezwa, na kama Mbosso anasikiliza namkaribisha sana BASATA milango ipo wazi ili aje kupata maelezo," alimaliza Mtumwa.