MSANII wa muziki wa kizazi kipya kutoka lebo ya Wasafi Mbwana Kilungi ‘Mbosso’ amesema baada ya kusikia taarifa za msiba za Rais wa awamu wa tano John Magufuli walishindwa kufanya video ya wimbo wake.
Mbosso alisema wakati wakiwa mtaani wanafanya video ya wimbo akiwa na bosi wake Nassibu Abdul ‘Diamond Plutnumz’ ghafla walipata taarifa hizo ikawalazimu kuacha kazi na kurudi studio.
Akizungumza Dar es Salaam alisema anamheshimu kiongozi huo kwani sehemu kubwa ya mafanikio yake kimuziki yamepatikana katika utawala wa Magufuli.
“Msiba ulinikuta nikiwa nachukua video ya moja ya nyimbo zangu na nilikuwa na Diamond ndio tukapata habari za msiba, tukajikuta tumeacha na kurudi studio,”alisema.
Nyota huyo alisema anakumbuka namna alivyovishwa kofia na Magufuli kipindi cha kampeni za Urais mwaka jana.
Alisema licha ya kiongozi huyo kuwaacha mapema, kama mtanzania anajivunia maendeleo yaliyoachwa katika sekta mbalimbali ikiwemo miundombinu, elimu, kuwasaidia wanawake na kuomba watanzania kumuombea rais Magufuli.