MWIGIZAJI wa filamu nchini Mohamed Fungafunga maarufu ’Jengua’ anazikwa leo saa saba mchana katika Makaburi ya Mburahati jijini Dar es Salaam.
Mkongwe huyo wa filamu amefariki dunia asubuhi ya Desemba 15 Mkuranga, mkoani Pwani.
Kwa mujibu taarifa iliyotolewa na mke wake Maua Ally, amesema mumewe ambaye amefariki akiwa nyumbani kwa mwanaye mkubwa, alikuwa akisumbuliwa na maradhi ya shinikizo la damu.
“Alikuwa anasumbuliwa na presha kwa hiyo tulikuwa Mkuranga kwa mtoto wake mkubwa kwa ajili ya kumuuguza, lakini leo tumeamka asubuhi hali ikawa mbaya na amefariki hapa nyumbani,” amesema Maua.
Umaarufu wa Jengua ulianza mwanzoni mwa miaka ya 2000 alipoigiza katika tamthilia zilizokuwa zikiandaliwa na kikundi cha Chemchemu Arts Group kupitia igizo la Kidedea.