Hatua hiyo imefikiwa leo wakati kesi hiyo ilipopangwa kwa ajili ya kusikilizwa ushahidi wa Jamhuri katika mahakama hiyo iliyoketi chini ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Rashid Chaungu.
Hata hivyo, upande wa Jamhuri umedai kuwa kesi hiyo ilipangwa kwa ajili ya kusikilizwa lakini hawana shahidi.
Hakimu Chaungu amesema upande wa Jamhuri hawana sababu ya msingi ya kutoita shahidi hata kama kesi hiyo ilipangwa kusikilizwa Mei 14, mwaka huu Siku ya Sikukuu ya Eid.
"Februari 22, mwaka huu nilitoa ahirisho la mwisho kwa kesi hii kwa sababu upande wa Jamhuri haukuwa na shahidi, Aprili 29, mwaka huu hakuna Shahidi aliyeletwa nikatoa ahirisho jingine la mwisho mpaka leo bado mmeshindwa kuita mashahidi" amesema hakimu na kuongeza.
"Kutokana na mazingira haya mahakama yangu inafuta mashtaka dhidi ya washtakiwa, inawaachia huru chini ya kifungu cha 225 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai" amesema Hakimu Chaungu.
Aidha, washtakiwa hao waliwekwa chini ya ulinzi wa askari polisi na kuwekwa mahabusu ya mahakama hiyo.
Awali, Kabla ya kesi hiyo kukutwa, wakili wa Serikali Silvia Mitanto aliieleza mahakama kuwa, wameshindwa kupata shahidi kwa kuwa kesi hiyo ilipangwa kusikilizwa Mei 14 ambayo ilikuwa sikukuu hivyo aliomba wapangiwe tarehe nyingine
Mbali na Idris mshitakiwa mwingine katika kesi hiyo ni Innocent Maiga anayekabiliwa na kosa la kushindwa kutoa taarifa ya mabadiliko ya matumizi ya laini ya simu kwa mtoa leseni kosa analodaiwa kulitenda kati ya Desemba 1, 2019 na Mei 19, 2020 katika eneo la Mbezi beach Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.