Mwanamuziki wa Bongo fleva, Dayoo hashikiki tena kwenye show kirahisi, amesema kitendo cha kumshirikisha Rayvanny katika wimbo wake 'Huu Mwaka Remix' kinaenda kuongeza thamani yake katika soko na kutoka kufanya show kwa Shilingi 6 milioni na kwenda bei ya juu zaidi.
Amesema ilikuwa ni ndoto yake siku moja kutengeneza wimbo mkubwa kama huo ambao utamfanya apige hatua kubwa kimuziki, kiuchumi na kichapaa, huku akiwasihi vijana wanaopambania ndoto na vipaji vyao kutokata tamaa.
Akizungumza na Mwananchi, Dayoo amesema 'Huu Mwaka' ulikuwa ni miongoni mwa nyimbo ambazo yupo nazo kwa muda mrefu ila ilitokea siku moja akiwa studio akaukumbuka na kuamua kuurekodi na sasa ni habari nyingine.
"Wimbo huu mwaka" umenipa mafanikio makubwa, umeniheshimisha lakini pia umenipa kolabo kubwa na Rayvanny hadi wasanii wengi wakubwa kuanza kuniamini, kwa hiyo naweza kusema ndiyo ngoma iliyonipa mafanikio makubwa zaidi tangu nimeanza muziki," anasema Dayoo.