Dar es Salaam. Kuna ukweli wowote kuhusu habari zinazosambaa katika mitandao ya kijamii kuwa msanii Harmonize amejiengua katika lebo ya Wasafi inayoongozwa na Diamond Platnumz.
Hakuna anayejua hilo lakini kuna baadhi ya kauli zilizotolewa na Diamond mwenyewe na mmoja wa mameneja wake zinaweza kutoa picha ingawa hakuna kati yao aliyethibitisha kuwa Harmonize ameachana na lebo hiyo.
“Kama Harmonize anataka kuondoka aondoke,” alinukuliwa akisema Diamond na baadaye kauli hiyo kuungwa mkono na mmoja wa mameneja wa Wasafi, Said Fella, “Kama akiamua kuondoka hakuna wa kumzuia.”
Huo ni mwanzo wa kile kinachodaiwa Harmonize anaweza kujitoa kwenye lebo ya Wasafi.
Lakini mara kadhaa Harmonize amekuwa akijibu kuhusu tetesi hizo, “Siwezi kuondoka Wasafi kwani namchukulia Diamond kama baba yangu ndio aliyenilea kimuziki.”
Tayari Harmonize anamiliki lebo ya muziki ya Konde Gang ambayo inafanya kazi zake kama ilivyo Wasafi.
Pia Soma
- VIDEO: Ali Kiba, Harmonize wapishana msiba wa Mbalamwezi wa kundi la The Mafik
- Baraza la Mawaziri Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kutangazwa wiki ijayo
- Zungu la unga Akasha alamba mvua 25 Marekani
Hivi karibuni Harmonize katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram aliondoa utambulisho wake kuwa chini ya Wasafi.
Kabla ya kuondoa utambulisho huo ilikuwa ikisomeka ‘Signed Under WCB Wasafi’ sasa ameondoa neno hilo na kuandika ‘WCB4LIFE’.
Harmonize hakuwepo katika ufunguzi wa tamasha la Wasafi lililofanyika Julai 19, 2019 katika Viwanja vya Zimbihile, Muleba mkoani Kagera na badala yake alijiunga nao jijini Mwanza kwa madai kuwa alikuwa na shoo nje ya nchi.