Dar es Salaam. “Sipo tayari kufanya mahojiano kwa sasa, kuna vitu vingi juu yangu vinaendelea ikiwamo kutajwa kwenye tuzo, nikiwa tayari kwa hilo nitakuambia” amejibu kwa kifupi msanii Harmonize.
Harmonize amejibu hayo leo Jumatano Oktoba 2, 2019 alipotakiwa kufafanua kuhusu alichopost kwenye mtandao wa Instagram kuwa anataka kuachia wimbo mpya hivi karibuni.
Staa huyo aliyeomba kuondoka kwenye lebo ya WCB ambayo aliingia nao mkataba wa zaidi ya miaka 10, siku za hivi karibuni amekuwa hasikiki kwenye vyombo vya habari zaidi ya kuachia nyimbo mbili za kushirikishwa nje ya lebo hiyo zikiwamo ‘Inabana’ aliyofanya na Eddy Kenzo na ‘Oyoyo’ aliyoshirikishwa na Skales.
Kwenye tuzo za MTV Europe Music Awards 2019, msanii Harmonize mshiriki pekee kutoka Ukanda wa Afrika Mashariki kuwania tuzo ya Best African Act.
Kwenye tuzo hiyo anapambana na wasanii kama Burna Boy, Teni, Nasty C, PrinceKaybee na Toofan kutoka Afrika Magharibi.
Tuzo hizo zinatarajia kufanyika Novemba 3, 2019 jijini London.
Pia Soma
- Mrembo Gigi avaana na aliyevamia jukwaa la Fashion Show
- Waziri Bashungwa akerwa na utendaji wa kiwanda cha Nyuzi Tabora
- Wamiliki kiwanda cha Nyuzi walalamikia ukosefu wa masoko
Kipengele kingine kitakachowaniwa siku hiyo ni msanii bora wa mwaka ambapo Harmonize atawashuhudia kina Ariana Grande, J Balvin, Miley Cyrus, Shawn Mendes na Taylor Swift wakichuana.
Katika orodha hiyo msanii ambaye ametajwa mara nyingi ni Ariana Grande ambaye ametajwa kwenye vipengele sita kikiwamo cha video bora, wimbo bora, Pop bora, mwimbaji bora wa laivu na msanii mwenye mashabiki wengi.