Dar es Salaam. Licha ya kutangaza kujiondoa katika lebo ya Wasafi , msanii Rajabu Abdul maarufu Harmonize bado hajamalizana na lebo hiyo.
Oktoba 24, 2019 katika kipindi cha XXL cha Redio Clouds, Harmonize alieleza jinsi alivyouza nyumba zake tatu na baadhi ya mali ili kuilipa lebo hiyo Sh500 milioni kwa ajili ya kupata hakimiliki ya kutumia nyimbo zake na jina.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumamosi Januari 18, 2020 meneja wa msanii huyo, Beauty Mmari maarufu Mjerumani amesema, “bado hatujamalizana nao, kuna vitu hatujavikamilisha kama ilivyoainishwa katika mkataba alioingia Harmonize na lebo hiyo.”
“Tukikamilisha na kumaliza suala hili kwa amani kama anavyotaka Harmonize, tutaliweka wazi kwa mashabiki wake na umma kwa ujumla,” amesema Mjerumani bila kutaka kuweka wazi mambo ambayo hawajamaliza hadi sasa.
Katika mazungumzo yake kuhusu mkataba na lebo ya Wasafi inayomilikiwa na msanii Diamond Platnumz, mkali huyo wa wimbo Uno na Kushoto Kulia, alieleza kuwa ulikuwa na kipengele cha kulipa kiasi hicho cha fedha ikiwa atavunja mkataba ili aweze kuendelea kutumia nyimbo pamoja na jina lake la kisanii.
“Mkataba ulinitaka nilipe Sh500 milioni na gharama za kuandaa nyimbo zangu zote wakati nikiwa chini ya Wasafi,” amesema Harmonize.
Pia Soma
- Rose Muhando: Wanaume hunikimbia, sitamani kuolewa
- Hiki ndicho kilichotokea mgahawa wa Harmonize unaotembea
- KIJIWENI LIVE: Kumbe Dogo Aslay ana busara kuliko Stamina